Monday, 3 September 2018

Usingoje Kesho

"....tazama,  wakati  uliokubalika  ndio  sasa;  tazama,  siku ya  wokovu ndiyo sasa.) 2 Wakorintho 6:2 “
Jana ni historia, kesho  ni siri, leo  ni zawadi kutoka kwa Mungu, ndiposa tunaiita present-zawadi.” —Bil Keane

Siku  moja  mwandishi  aliyeitwa  Leo  Buscaglia  alisimulia  hadithi kuhusu  mama yake na kile alichoita “chakula cha jioni  cha familia na cha mateso.” Ulikuwa usiku  ule  wa kwanza baada  ya  baba  yake kurudi nyumbani  na akasema kwamba inaonekana kana kwamba itabidi  afilisike  kwa  sababu  mwenzi  wake  kibiashara  alikuwa ametoroka na pesa  za kampuni.  Mama yake  Buscaglia  alienda kuuza  vito ili anunue chakula kwa  ajili ya karamu ya kukata na shoka.  


Baadhi ya watu  wa familia  walimkemea  kwa kuuza vito na kutumia  pesa  nyingi  sana.  Lakini  yeye  akawaambia,  “ Wakati  wa furaha ni sasa, wakati ambao tunaihitaji zaidi, na si wiki ijayo.”1 Ninapongeza  hatua  hiyo  ya  ujasiri na hekima ya  mama huyu. Matumaini na furaha  ni mambo mawili ambayo hayapaswi  kuahirishwa  kamwe.  

Watu wengine huishi  maisha yao wakingoja “kesho.”  Husema, “Pengine kesho  mambo yatakuwa  bora  zaidi,”  au  “Natumaini  wakati  wote  kuna  kesho,”  au *“Natamani hii siku iishe na niione siku ya kesho.”* Wakati  mtu  anapoahirisha  matumaini  hadi  kesho,  hapati  furaha ya  leo,  na  hayo  siyo  maisha  yaliyomfanya  Yesu  afe  msalabani. 

Yesu anataka tufurahie maisha yetu leo na kila siku. Amani,  raha, furaha, kujiamini,  ujasiri, afya, akili timamu, kibali,  baraka,  ndoa  thabiti—haya  yote  ni  mambo  ambayo  Mungu anapenda  uanze kuyapokea leo. Kila wakati unaposema moyoni, Naona  leo  itakuwa  siku  ya  hasara  kabisa;  pengine kesho  itakuwa  bora  zaidi, unakosa  mpango mzuri zaidi wa Mungu juu ya maisha  yako. Ikiwa Mungu  yuko  pamoja  nawe  leo— na  kweli  yuko  pamoja  nawe;  *Yuko nawe  wakati  wote—huna  haja  ya  kusubiri  wakati  fulani  ujao  ndipo uanze  kufurahi. 

Unaweza kupokea maisha yaliyojaa furaha,  ushindi na  utele  leo.  Mtume  Paulo  alisema  kwamba  wakati  kungali  LEO, sharti  tumsikie  Mungu na tusiifanye  mioyo yetu  kuwa migumu dhidi  ya  ahadi  zake  (Waebrania  3:15).  

Mungu  anafanya  kazi  katika maisha yako  leo,  na anataka uamini  leo  na ufurahi  leo! Zaburi  118:24,  inasema,  “Siku  hii  ndiyo  aliyoifanya  BWANA, Tutashangilia  na kuifurahia” (imeongezwa  msisitizo).  Mungu aliifanya  siku  hii kwa sababu fulani.  Kuna kitu maalum anachotaka kufanya.  Je,  uko  tayari  kukipokea?  Natumai  watu  hufanya  kile kinachoagizwa  na  kifungu  hicho:  Hushangilia  na  kuifurahia. Haijalishi hali ya hewa iko  namna gani huko  nje, jinsi  wanavyohisi, yale  yanayosemwa na watu, kuna vizuizi  vinavyowakabili, au  habari zinazotangazwa  na  vyombo  vya  habari—watu  wenye  matumaini husema,  “Bwana  ameiumba  siku  hii  ya  leo  kwa  sababu  fulani— Nitashangilia  na  kufurahi.Nitakuwa  na  matarajio  mazuri  kwamba Mungu atatenda kitu kizuri maishani mwangu leo!” 

Hebu niwasimulie hadithi inayonihusu mimi mwenyewe: Mnamo mwaka 2015  nilifikia  kiwango  cha  kukata  tamaa  kuhusu  hali  yangu ya  maisha.  Nilidhani  hakuna kitu  kizuri  kingetokea kwangu. Ingawa nilikuwa Mkristo,  sikuwa  ninapata  ushindi maishani mwangu. 

Siku moja  nilipokuwa  nimepanda gari  kwenda  kazini  mwezi  Februari mwaka  huo, nilimlilia Mungu katika hali ya kushindwa nifanye nini na  nafikiri  kwa  mara  ya  kwanza  katika  maisha  yangu  ya  Ukristo niliwahi kupitia  kitu kilichonifundisha  imani haswa  ni nini. Mungu alinihakikishia  moyoni mwangu kwamba  alikuwa anashughulikia hali yangu. Ingawa hakuna kitu kilichobadilika mara  moja katika hali  yangu,  lakini  baada  ya  hapo  nilikuwa  na  amani  kamili.  Nilijaa matarajio  mazuri  kwamba  kitu  kizuri kilikuwa kinaenda  kutokea siku  hiyo!    Nilikuwa  na  matumaini  ya  kweli!  Sikujali  Mungu  alifanya nini, au hata  alikifanya wakati  gani, kwa sababu moyoni mwangu nilijua  tayari  imetendeka.  

Ninaweza  kusema  wazi  kwamba  kuanzia wakati  huo na kuendelea, mambo yalianza kubadilika katika maisha yangu. Hayakuwa  kamili kwa  vyovyote, lakini kidogo kidogo, siku hadi siku, mambo mazuri yalianza kutokea. 

Ninajua  unaweza  kuwa  unasema  hivi:  “Jimmy  na  je,  ikiwa ninaamini  kitu kizuri  kitatokea leo na kisha  kisitokee?” Kwanza kabisa, hebu niseme kwamba ninaamini kwa dhati  ya  kwamba kitu kizuri  hutokea kila siku,  lakini  huenda tusikione. Pili, mambo mazuri yanayotokea  huenda  si yale  tuliyotarajia  haswa, lakini matumaini yalitupatia siku  nzuri  zaidi kushinda  kile ambacho  tungepata bila  matumaini,  kwa  hiyo  hilo  pekee  ni  jambo  zuri.  

Na  mwisho, nitasema kwamba sharti uamke tena  kesho  ukiwa na matumaini, ukiamini kwamba  kitu  kizuri  kitatokea  kwako siku  hiyo. Haijalishi utafanya hivyo kwa  siku  ngapi, endelea  kufanya hivyo, na utaona kwamba Mungu ni mwaminifu!!.

No comments:

Post a Comment