Wednesday, 29 August 2018

Nguvu za Kuendelea Mbele

Nakumbuka  siku  moja  nilipokea  habari  mbaya  sana  muda  mfupi kabla kuaanza kongamano la siku  tatu. Ilikuwa vigumu kuendelea, lakini  nilijua  sina  budi  kuendelea.  Nilihisi  Roho  Mtakatifu  akisema, “Nyanyua  mguu  wako  na  upige  hatua  kwenda  mbele.  Endelea kwenda Mbele!”

Kuendelea  kwenda  mbele  hakukuondoa  uchungu wote  na hali ya kuvunjika  moyo niliyohisi,  lakini  kulinizuia  nisiweze kuzama katika kilindi cha kukata tamaa,  na baada ya majuma machache, hali iliweza kutatuliwa.  Moja ya dalili  za ukomavu  wa kiroho ni kuwa  na nidhamu ya kutimiza ahadi zako, hata ikiwa  unapitia wakati  mgumu.  Nilikuwa  naumia,  lakini  nilihitaji  kuendelea kuwahudumia wengine  waliokuwa wanaumia,  na nilifanya  hivyo, Mungu aliniponya na kusuluhisha tatizo langu.


Hata  hali  iwe  ngumu namna gani kumbuka tunapoumia, mambo  huja  na  yakafikia  mwisho.  Majira  ya  kiangazi  wakati  wote huja baada  ya  majira  ya  baridi.  Jua  huwaka tena  baada  ya  dhoruba. Jana  kulitanda  mawingu kutwa nzima, na hatimaye  tukapata ngurumo za radi  na mvuka  kubwa,  lakini leo  anga ni la samawati na  jua  linawaka.

Nafikiri  tunaweza  kuona,  hata  katika  mifumo  ya kawaida ya hali ya hewa na mabadiliko ya majira, jinsi  ambavyo mambo yalivyo mabaya yanavyotoa  njia ya mambo mazuri.  Ikiwa mawingu yametanda  na kuna dhoruba  maishani mwako leo, tazamia  kwa hamu jua ambalo yamkini  litang’aa kesho, siku itakayofuata  au siku  itakayofuatia  ya pili.

Dhoruba haitadumu milele! Biblia inatoa mfano wa mwanamke mgonjwa (mwanamke aliyetoka  damu) aliyepita  katika  mkutano  kwa nyuma  ili amfikie  Yesu  (Marko  5: 25-34; Luka  8:43-48).  Hata  ingawa  mwanamke  huyu  alikuwa  ameugua kwa miaka 12 na kumaliza pesa  zake zote  kwa waganga ambao walishindwa kumsaidia,  alikataa  kukaa tu,  bila  kufanya chochote akisubiri  uchungu umwondokee. Aliamua kuruhusu  matumaini yamhamasishe  kupita katika kila tatizo.

Hakuna kitu ambacho kingemzuia  asimfikie  Yesu—si  kundi  la  watu,  si  ugonjwa,  si muda ule  mrefu aliosubiri, si mashaka  yake, si uchungu wake. Aliendelea  kusema moyoni mwake  Nikigusa  tu upindo  wa  vazi  lake nitapona  (Mathayo  9:21).  

Aliendelea  kwenda  mbele,  huku  akiwa  na matumaini na imani moyoni mwake. Huenda una kundi lako la  watu  unalopaswa kulipenya leo. Huenda ni kundi  la mawazo mabaya. Huenda ni kundi  la uchungu na maumivu  ya zamani. Huenda ni  kundi  la watu waliokaribu yako  wasiotaka  kukusaidia. Huenda ni  kundi  la matatizo ya kifedha. Huenda ni   kundi la uchungu mwilini mwako.

Lakini ukipita katikati ya mambo hayo yote  na ukakataa  kuruhusu  mambo ya kuvunja moyo maishani  yakukwamishe  katika kilindi  cha kuvunjika  moyo na shida, utaupata ushindi wako.

Wafilipi 3:13-14 inasema: Ndugu, sijidhanii  nafsi  yangu kwamba  nimekwisha  kushika;  ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo  mbele;    nakaza  mwendo,  niifikie  tuzo  la  thawabu ya  mwito  mkuu wa  Mungu  katika  Kristo  Yesu.

(imeongezwa msisitizo) Napenda  fungu  hili  la  Maandiko. 
Paulo  alisema  anayasahau yaliyopita—makosa  na  uchungu  wa  maisha  yake  ya  awali—na alikuwa  anakaza  mwendo  kwenda  mbele  kuifikia  hatima  yake. Unaweza  kufanya vivyo hivyo. Unaweza  kupita mambo hayo yote yanayoweza  kukuzuia  usiende  mbele. 

Leo  unaweza  kukataa  kuwa na  mtazamo  wa  kushindwa.  Leo  unaweza  kukataa  “kujifanya kifaurongo.”  Unaweza  kuchagua  kuendelea  kwenda  mbele— unaweza kuchagua kukaza mwendo.

No comments:

Post a Comment