Monday, 28 May 2018

AINA ZA MAOMBI

 

Kwanza kabisa  basi,  naomba  dua, sala,  maombi  na sala  za  shukrani zitolewe kwa Mungu kwa ajili ya watu wote. Kwa ajili ya wafalme  na wote wenye mamlaka,  ili tupate kuishi maisha ya utulivu  na amani pamoja na uchaji wa Mungu na mwenendo mwema. Jambo hili ni jema na lampendeza Mungu Mwokozi wetu. 1 Timotheo 2:1-3


Kama tunavyoona katika  maandiko haya, tunafaa  kuomba kila aina ya maombi tukijiombea na kuwaombea wengine pia. Hebu tuangalie aina tofauti ya maombi ambayo inafaa kuomba tunapoanza kujifunza kuomba kwa moyo bila kukoma. Ombi la kujitolea umkabidhi BWANA njia yako, pia umtumaini, naye atafanya. Zaburi 37:5. 

Kwanza kuna maombi ya kujitolea
Hapa tunayatoa  maisha yetu na kumkabidhi Bwana.  Tunafanya hivyo tunapompa hofu  zetu. Kama tunavyoambiwa katika  1 Petro 5:7 “…Mwekeeni matatizo yenu yote, maana yeye anawatunzeni.” 

Wakati tunapokumbwa na hofu ya mambo  na shida  ambazo zinatishia kutuangamiza, tunahitaji kuomba: “Bwana, mimi sitaubeba  mzigo huu wa matatizo na kuukubali unitese na kunizuia  kukutumikia.  Baba ninaomba sasa hivi kwamba utanipa nguvu na kuniwezesha kufanya yale ambayo umeniitia kufanya hata kama nitayafanya nikiwa mwenye hofu. Ninakuwekea shida  hii, chochote kiovu, kibaya au cha  kuchukiza, ambacho shetani anajaribu kunionyesha kwamba kitanitokea.  Ni shauri lako, si langu kwa maana nitafanya yale uliyoniambia na nikuachie hayo mengine.” Iwapo tutaomba mara tu hofu inapojitokeza— basi tutaona hofu hiyo ikishindwa kwa nguvu za Mungu. 

Shida  ni kwamba, si  hofu kubwa ambazo hututatiza sana.  Mara nyingi ni hofu  ndogondogo  ambazo  hutuandama  usiku  na  mchana ndizo  hutuibia uzima  na furaha yetu kama vile mbweha wadogo ambao huharibu mizabibu (Wimbo 2:15). 

Ndio  maana,  unapohisi  hofu,  hata iwe  ndogo  kiasi  gani, unahitaji kuomba, “Bwana, sitaishi kwa hofu. Badala yake,  ninakukabidhi maisha yangu na ninakuomba ushindi juu ya jambo hili ambalo linajaribu kunitesa na kunizuia kuishi maisha kamili ambayo unatamani niishi na kutimiza  mpango wako mzuri na mkamilifu.” Iwapo tutaomba hivyo kwa moyo na dhati, basi Bwana ataheshimu maombi  yetu na kujitoa kwetu na atatimiza sehemu  yake ya kutuweka huru. Maombi ya Kujitakasa au Kujiweka Wakfu Kwa hiyo, ndugu zangu,  maadam Mungu ni mwenye huruma nyingi, nawasihi kwa moyo wote: jitoleeni nafsi zenu kwa Mungu kama tambiko iliyo hai, takatifu na yenye kupendeza.

Hii ndiyo njia yenu halisi ya kumwabudu. Warumi 12:1 Wakati tunapokitoa kitu kwa Mungu katika maombi,  hilo huwa ombi la kuweka wakfu. Tunapofanya hivyo tunasema, “Bwana, ninakupatia  pesa zangu, wakati wangu, nia yangu”—  chochote kile tunachomtolea Bwana.
Mtume Paulo anatuhimiza katika maandiko haya tutoe, na kuweka wakfu miili  yetu kwa Bwana,  viungo  vyote vya miili  yetu vipate kumtumikia, ambayo ndio njia yetu halisi ya kumwabudu. Sisi  pia huomba ombi la kuweka wakfu wakati tunapowatoa watoto wetu kwa Bwana, tukiahidi “…kuwalea katika kumcha na kumheshimu Mwenyezi—Mungu.” (Waefeso 6:4). 

Jinsi tunavyoweka wakfu maisha yetu, pesa na mali yetu, nia na miili yetu, jamii na watoto wetu kwa Mungu, ndivyo pia tunafaa kutoa na kuiweka wakfu midomo  yetu—na kufanya hivi kunatuongoza katika aina ifuatayo ya maombi.

Maombi ya Sifa na Ibada
Basi, kwa njia ya  Yesu, tumtolee Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani sifa zinazotolewa na midomo inayoliungama jina lake. Waebrania 13:15 Nafikiri  sote  tunafahamu  sifa  na  ibada.    Sifa  ni  kuyarudia mema ambayo Mungu amefanya. Ni kusema hadithi ya mema aliyotufanyia. 
Ibada  ni kumsujudu.  Ni kutambua “Kustahili” kwake. Ni  kumtambua  Yeye na  utukufu wake.   Hii  ndio  sababu mwandishi wa kitabu cha  Waebrania anatuambia kwamba inafaa tumsifu na kumwabudu Mungu kila wakati.  

Kama tulivyoona, ombi la sifa na ibada linatakiwa kuwa kama kupumua, mchana na usiku, kila wakati.  Tunatakiwa kuwa na shukrani kwa Mungu kila wakati. Tukitambua, tukikiri  na kulitukuza  Jina lake katika maombi, sifa na ibada. 

Maombi ya Shukrani
Na muwe na shukrani katika  kila hali. Hayo ndiyo anayotaka Mungu kwenu katika kuungana kwenu na Kristo  Yesu. 1 Wathesalonike 5:18 Mara  tu baada ya kutuambia katika 1 Wathesalonike 5:17 tuombe bila ya kukoma, Mtume Paulo anatuelekeza  tumshukuru Mungu katika  kila jambo.

Haijalishi kinachoendelea katika  maisha yetu kwa maana hili ndilo kusudi la Mungu kwa ajili ya maisha yetu. Jinsi maombi yanavyopaswa kuwa mtindo wa maisha  yetu, ndivyo shukrani inapaswa kuwa sehemu ya maisha yetu. Kumshukuru Mungu hakupaswi kuwa jambo  ambalo tunafanya mara  moja  kwa  siku  tunapoketi  chini  na  kujaribu  kufikiri  mambo yote mema  ambayo Mungu ametufanyia, na kusema  kwa udhaifu, “Asante Bwana.” Hiyo  ni  dini,  jambo  ambalo  tunafanya  kwa  sababu  tunafikiri kuwa Mungu anatuhitaji tumfanyie.  Shukrani ya kweli huendelea kububujika  kutoka kwenye moyo ambao umejaa shukrani na sifa kwa Mungu kwa sababu  ya utukufu  wake na matendo yake. 

Si jambo tunalofanya ili atutimizie hitaji fulani, tupate  kibali,  tupate ushindi, au ili tuhitimu kuweza kupata baraka. Aina ya shukrani  ambayo Mungu Baba anatamani kutoka  kwetu ni ile ambayo imechochewa  na Roho  Mtakatifu ndani  yetu ambaye anatuvuta tumweleze Bwana yale tunayohisi katika roho zetu. Shukrani ya kweli ni ile iliyoelezwa na mwandishi  wa Zaburi aliposema: “Mshukuruni Bwana wa mabwana, kwa maana huruma zake na fadhili zake zadumu milele—” (Zaburi 136:3)!

Maombi katika Roho
Lakini ninyi, wapenzi wangu, endeleeni kujijenga kikamilifu katika imani yenu takatifu. Salini kwa nguvu ya Roho Mtakatifu. Yuda 20 Tulikuwa tayari tumeona katika  waefeso 6:18 kwamba haitoshi kuomba maombi ya kila aina bila kukoma tu, bali jinsi tunavyoambiwa na  Yuda, maombi yetu yanafaa kuwa “katika Roho Mtakatifu.” 

Ni Roho  Mtakatifu wa  Mungu  ndani yetu ambaye hutuchochea  na kutuongoza kuomba. Badala  ya kusubiri, mimi  na wewe tunahitaji kujifunza kujitoa kwa Roho Mtakatifu mara tu tunapohisi mwongozo  wake.  Hii  ni  sehemu  ya kujifunza kuomba kila aina ya maombi kila wakati, popote tulipo, hata tunapokuwa tukifanya chochote. Mwito wetu  unafaa kuwa ule wa tenzi  ya kitambo  iliyosema, “Kila nitakapohisi Roho Mtakatifu akinichochea moyoni, nitaomba.” Iwapo tunajua tunaweza  kuomba wakati  wowote, mahali popote, basi hatutahisi tunalazimika kungoja hadi wakati na mahali maalum ili tuweze kuomba. 

Maombi ya Kukubaliana
Tena nawaambieni, wawili miongoni mwenu wakikubaliana  hapa duniani kuhusu jambo lolote la kuomba, Baba yangu  wa mbinguni atawafanyia jambo hilo. Kwa maana popote  pale wanapokusanyika  wawili au watatu  kwa jina langu, mimi nipo hapo kati yao.”
Mathayo 18:19,20 Kuna nguvu katika kukubaliana.  Biblia inatuambia kwamba iwapo Bwana  yu pamoja  nao,  mtu mmoja  anaweza  kuwapiga elfu moja,  na wawili  wanaweza kuwapiga elfu kumi. (Kumbukumbu 32:30).

Lakini nguvu hii  inapatikana tu wakati tunakuwa katika makubaliano na wenzetu—pamoja na Bwana. Ni wazi kwamba hatuwezi kugombana na wenzetu kila wakati na kisha tukubaliane katika  maombi kuhusu hitaji fulani na tutarajie kwamba “Ombi  la  kukubaliana”  litakuwa na nguvu –  ndivyo tunavyoonywa katika 1 Petro 3:7 (UNION): 

“Kadhalika nyinyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama  chombo  kisicho  na  nguvu;  na kama  warithi pamoja  wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe.” Vivyo hivyo, hatuwezi kunung’unika na kumsengenya mhubiri wa neno wiki nzima na kisha tumwendee kwa maombi kuhusu shida fulani ambayo imetukumba  na tutarajie  kwamba  ataomba ombi la makubaliano pamoja nasi. Kwa nini? Kwa sababu tayari hatumo katika makubaliano na wenzetu na Mungu. Unajua  ni  kwa nini Mungu  anaheshimu  maombi  ya kukubaliana? Ni kwa  sababu  anajua kuwa  si jambo rahisi kwetu  kutembea  na kuishi katika makubaliano na wengine. Mungu anamheshimu mtu yeyote ambaye amejitoa kufanya hivyo. Mimi  na wewe tukikubaliana na wenzetu na Mungu pia, basi maombi yetu yatakuwa yenye nguvu na uwezo zaidi. Maombi ya pamoja “Hawa wote walikusanyika pamoja kusali…”

Matendo 1:14 Kuna nguvu  kubwa katika maombi  ya pamoja,  ambayo ni  aina mojawapo  ya ombi  la  kukubaliana kama  inavyodhihirika katika mstari huu tuliosoma.  Katika  kitabu  cha Matendo, tunasoma kwamba watu wa Mungu walikuja, “wakakusanyika pamoja”  (Matendo  2:1, 46, 4:24, 5:12, 15:25). Katika  Wafilipi  2:2,  tunaambiwa  na  mtume  Paulo,  “Ikamilisheni furaha yangu kwa kuwa na nia, moja, kusudi moja,  na upendo mmoja.”

Iwapo tutayafuata maneno haya na tuishi na kukubaliana  na wenzetu na Mwenyezi Mungu, tutaona matokeo ya ajabu kama walivyoona wafuasi wa kwanza katika kitabu cha Matendo. 

Maombi ya Maombezi
Kwanza kabisa, basi naomba dua, sala, maombi na sala za shukrani zitolewe kwa Mungu kwa ajili ya watu wote. 1 Timotheo 2:1 Kumfanyia mtu maombezi, ni “Kusimama pengoni kwa ajili yake.” Ni kumwombea mbele ya kiti cha enzi cha Mwenyezi Mungu.
Katika Warumi  8:26,27, tunaambiwa na mtume  Paulo  kwamba Roho Mtakatifu hutuombea kulingana na mapenzi ya Mungu. 

Katika  Waebrania  7:25 tunasoma kwamba Yesu “…anaweza daima kuwaokoa kabisa wote wanaomwendea Mungu kwa njia yake, maana yeye anaishi milele kuwaombea kwa Mungu.” Mwishowe, Paulo anatuhimiza hapa katika  1 Timotheo 2:1, tuwafanyie maombezi  watu wote.  Kumaanisha  kwamba tunatakiwa kuwaombea watu wote kila mahali.
Maombezi ni mojawapo ya njia muhimu kabisa katika  kuendeleza huduma ya  Yesu aliyoianzisha hapa duniani. 

Maombi ya Kukaa Kimya
…Bwana yu hekaluni Mwake; dunia yote na iwe kimya mbele zake. Habakuki 2:20
Mimi huita aina hii ya maombi, “kumngojea Bwana.” Daudi alijua kuhusu kumngoja Bwana kama tunavyoona  katika Zaburi 27:4 alipoandika:
“Jambo  moja  ninalitamani, kwamba nikae nyumbani  mwa Bwana siku zote za maisha yangu,  niutazame uzuri wa Bwana na kutafakari katika hekalu mwake takatifu.” Ni muhimu sana kujifunza kumngoja Bwana kwa sababu watu wengi hawaelewi  kwamba ni  muhimu  kufanya hivyo  katika maombi. Maombi si jambo tunalofanya  tu, bali pia ni kuwa na nia ya kungoja. Maombi  si  kumzungumzia Mungu kila wakati—ni kumsikiza pia.

Maombi ya Mahitaji Binafsi
Msifadhaike juu ya jambo lolote; lakini katika kila jambo mjulisheni Mungu haja zenu, kwa kusali na kuomba pamoja na kushukuru. Wafilipi 4:6 Ombi la kibinafsi ni kumwomba Mungu akutane na mahitaji yetu. Mimi husema kwamba  ombi kuu  kabisa  ambalo mtu yeyote anaweza kuomba ni ombi ninaloliita, “Ombi la Nisaidie”. “Mungu nisaidie, nisaidie, Ee Mungu nisaidie!”
Mimi huliomba sana. Wakati mwingine mimi  huamka usiku wa manane  kwenda kujisaidia, na sina shida yoyote;  bali  ninajikuta  ninaomba, “Ee Mungu, nisaidie, nisaidie  mimi!”  Ninaamini ni Roho  Mtakatifu aniongozaye kuomba hivyo. Ombi hili la “Mungu nisaidie” ni ombi lenye nguvu sana. Iwapo mimi  na  wewe  tumefika  mahali  ambapo  hakuna  la  ziada  tuloweza kufanya, tunaweza kuomba hivi. Ombi lingine la kibinafsi ni lile ninaloliita, “Bwana, Nakuhitaji.”
Tunaweza  kuona mabadiliko  makubwa katika maisha  yetu iwapo tutaacha kujaribu kufanya kila kitu kwa nguvu zetu wenyewe. Mithali 3:5-7 inatuambia:  “Mtegemee Bwana kwa moyo wako wote, naye anainyosha  njia  yako. Usiwe  mwerevu  machoni  pako, bali mche na kumwabudu Bwana na kuachana na maovu.” Usingoje  mpaka wakati utakapokuwa umeshindwa  na kutambua kwamba  huwezi kushinda peke  yako  ndipo umkimbilie Mungu akusaidie.

Tambua kabla  hata hujajaribu, kwamba huwezi lolote kwa nguvu zako. Mtegemee Mungu kabisa. Jifunze kuomba hivi: “Bwana, siwezi kufanya  jambo hili, lakini wewe  unaweza kwa kunitumia mimi.  Ninakutegemea na kukutazamia, nikiwa na tumaini ndani yako kwa moyo wangu wote. Nisaidie Bwana, kwa maana ninakuhitaji.” Ombi  hilo dogo linatosha kukuwezesha kushinda hali mbaya mno maishani. Kutambua  kuwa  Mungu ndiye msaada wetu huchukua muda  mfupi sana  lakini kunaweza kutusaidia kushinda  kushindwa  katika hali za  maisha  yetu ya kila siku—hasa tunapogundua kwamba bila Bwana hatuwezi chochote. Unaposema,  “Bwana,  ninakutegemea, nisaidie  tafadhali,” umeomba ombi la kibinafsi—nalo lina nguvu. Haya ndiyo maombi  tunayotakiwa  kuomba tunapowasilisha  hitaji la aina yoyote.

Tumia kanuni hii: jiambie; “Jinsi ninavyoendelea kuwa na shughuli nyingi, ndivyo ninavyohitaji  kutumia  muda mwingi na Bwana.”  Kwa sababu jinsi  nilivyo na mengi ya kufanya, ndivyo ninavyohitaji msaada zaidi kutoka kwake. Ukiwa mtu wa shughuli shughuli kama Martha kiasi cha kwamba huna wakati  wa kukaa  na Bwana, basi wewe una shughuli kupita kiasi. Unahitaji kuwa kama Maria na ujifunze kuachana na mambo mengine yasiyo ya maana sana ili upate kukaa miguuni pa Bwana na kujifunza kutoka kwake. Ukifanya hivyo, basi utapata funguo za ufalme kutoka kwake!

No comments:

Post a Comment