Kama umekuwa ukingoja kwa muda mrefu na hujaona ukipiga hatua za kwenda mbele, haikosi unaanza kuwa mchovu sana kwa kungoja. Nataka kukutia moyo kufanya upya nia yako kuhusu kungoja.
Katika Marko 4:20-27 Biblia inasema kwamba yafaa tuwe na subira kama mkulima awekaye mbegu yake kwenye ardhi kisha anaingoja mvua ya awali na ya baadaye. Neno linaendelea kusema kwamba aingojeapo mbegu kumea, yeye huamka na kulala, na mwishowe mbegu ile humea. Naye, mkulima hajui inavyotendeka.
Mungu amenifundisha kupitia kwa andiko hili kuendelea kuishi maisha niliyo nayo sasa nikiwa ninayangojea mambo niliyo nayo moyoni kuja kuoenekana na kutimia. Tunaweza kuwa tumetilia mkazo sana kujaribu kuzalisha kilicho mbele yetu kiasi cha kwamba tunasahau kuchunga na kufurahia tulicho nacho mkononi. Mimi nilikuwa na maono kutoka kwa Mungu miaka kumi kabla sijaanza kuyaona yakitimizwa. Katika muda wa miaka hiyo, naamini nilikosa furaha nyingi huku nikijaribu kuzalisha kitu hicho nje ya wakati ulioteuliwa na Mungu.
Tuseme mwanamke aliye na watoto watano atunge mimba na kuwa mja mzito. Kama angelijaribu kumzaa yule mtoto wa sita katika mwezi wa kwanza wa mimba ile, hilo lingeonekana jambo la kipumbavu.
Na je, kama angejishughulisha sana kumzaa yule mtoto kiasi cha kukosa kuwachunga ipasavyo wale wengine watano alio nao tayari? Tunaweza kuona kwa urahisi na wazi upumbavu wa kitendo kama hicho.
Ukweli ni kwamba, watu mara nyingi hufanya jambo sawa na hilo katika hali zingine. Furahia mahali uliko ukingojea kufika mahali unataka kwenda! Biblia inaposema kwamba mkulima huamka na hulala, naamini inamaanisha yeye huendelea kuishi maisha yake ya kwaida kila siku, huku akingoja shamba lake lijae mimea iliyochipuka jinsi anavyotarajia.
Siku moja, mchungaji fulani alitupokea katika uwanja wa ndege uliojaa umati wa watu. Kazi aina mbali mbali zilikuwa zinaendelea kila mahali. Vifaa vya kupanda ngazi vilikuwa na milolongo, na mikahawa ilikuwa na milolongo. Ilionekana kana kwamba popote tulipogeuka tulikuwa tunangoja tu. Nikaona kwamba mchungaji yule alikuwa ameanza kuudhika na hali hiyo. Mara tu alinigeukia na kusema, “Nadhani unaweza kuona kwamba singojei vyema.” Wakati wowote hatujangojea vyema, matokeo ni wazi, sio tu katika mienendo yetu inayojidhihirisha katika hisia zetu, bali pia katika miili yetu. Kungojea ni sehemu kubwa sana ya maisha, na kama kungojea kila mara huleta masumbuko moyoni, matokeo yake ni kwamba huleta wasiwasi ambayo mwishowe huidhuru miili yetu na yenye uwezo wa kuleta magonjwa. Mchungaji huyo ambaye hakuwa “anangoja vyema” alikuwa mgonjwa sana wakati huo na ugonjwa amabao dakatri alisema ulikuwa umeletwa na miaka mingi ya kuishi na wasiwasi nyingi. Fanya upya nia yako kuhusu kungoja, nawe hutauona ugumu kungoja. Kusema kweli sisi hutumia muda mwingi maishani mwetu tukingojea kuliko muda tunaotumia kupokea. Baada ya kupokea tulichokuwa tukingojea, tutaanza kungojea kitu kingine.
Kama unaweza kuona ninachomaanisha, utaona kwa haraka kuwa kungojea ni sehemu kubwa ya maisha. Tuseme kwa mfano upate nyongeza ya mshahara, kisha uanze kungoja nyingine.
Unangoja kupata mtoto, kisha unaanza kungoja mtoto huyo awache kutumia nepi na aanze kutumia surwali ndefu, na muda si muda unaanza kungoja aanze kujinunulia surwali ndefu zake yeye mwenyewe! Unangoja kununua nyumba, kisha unaanza kungoja kununua vyombo vya nyumba ile ambayo huingojei tena.
Kisha unangoja kumpata msichana wa kazi ya nyumbani kukusaidia kusafisha nyumba na vyombo vyako ulivyongojea kupata. Je unaelewa ninachomaanisha? Jifunze kufurahia kungoja, ukifahamu ya kwamba kungoja ndiko kutakakokufikisha ndoto yako. Yafaa niseme kuwa “kungoja vyema” ndiko kutakaokufikishia kwenye ndoto yako. Kutimizwa kwa ndoto hiyo, bila shaka kunatoka kwa Mungu, lakini kungoja ni kama kijana yule anayetumwa kufikisha ujumbe mahala fulani. Wakati mwingine, mtu huanza kungojea jambo fulani kutimika, lakini wakati kijana yule anyetumwa kumfikishia ujumbe anapofika, tiyari wameshaondoka na kwenda kuanza jambo lingine, na huenda wasiwepo kuona kutimilika kwa jambo hilo jipya pia. Watu wasio na subira mara nyingi huwa hawatulii kiasi cha kutosha kuona mwisho wa mambo makuu kweli, maana mambo makuu huchukua muda mrefu kutimia kikamilifu.
Rafiki yangu kila mara husema, “Cha haraka ni dhaifu, cha pole pole ni kizima kama kigongo.” Kama kitu kimefanywa kwa haraka kuwafaa wale wasio na subira na wasio na uwezo wa “kungoja vyema”, huenda hakitadumu.
Lakini ikiwa watu wako tayari kungojea wakati ulioteuliwa na Mungu, kitu hicho kitaundwa sawa sawa na kitadumu na kudumu kwa muda mrefu. Mara kwa mara sisi huona “nyota zinazofyatuka” katika huduma watu ambao hutokea ghafla, kutoka mahali ambapo hapajulikani na muda si muda wanajulikana ulimwengu mzima, mara nyingi kwa sababu waliweza kuingia katika kikundi cha watu ambao waliwafungulia milango. Huduma kama hizi nadra husitawi.
Mara nyingi hizo huwa na matatizo ya kifedha au ya kitabia kwa sababu utu wema hujengwa katika nyakati zile ngumu za kungojea, lakini wao hawakupitia wakati huo wa kujenga tabia na utu wema. Kama mtu akiepuka nyakati zile ngumu na kufyatuka mara moja, kwa kawaida hatadumu. Marko 4:5, 6 husema kwamba mbegu ile inayoota kwa haraka kana kwamba ni kwa usiku mmoja huungua jua linapozuka. Mwishowe tunapofikia kiwango cha kukubali na kuheshimu nyakati za kungoja, Mungu huanza kufanya kazi murua kwa makini kabisa ndani yetu. Na hata ingawa hatuoni ni nini kinachotendeka, mambo yatakayo tufurahisha baadaye yanaendelea sasa hivi bila ya kuonekana.
No comments:
Post a Comment