Monday, 28 May 2018

OMBA KUHUSU KILA KITU,USIOGOPE CHOCHOTE..


Sala ya mtu mwema ina nguvu ya kutenda mengi… Yakobo 5:16
Wakati mmoja,  Bwana alinizungumzia maneno haya; “Omba kuhusu kila kitu,  na usiogope chochote.”  Aliniambia hivi nilipokuwa na hofu kwamba kinyozi wa nywele ambaye nilikuwa nimemwendea kwa mara ya kwanza hangeweza kutengeneza nywele zangu vizuri.
Roho  Mtakatifu alinizungumzia, “Usiogope hali hii. Wewe iombee. Omba kwamba Bwana atampa upako kinyozi huyu ili aweze kufanya kile kinachohitajika.”


Kisha katika majuma yaliyofuatia, Bwana aliendelea kunionyesha mambo tofauti kuhusu vile maombi yanavyoishinda hofu.

Mengi yao  yalikuwa ni  maeneo  madogo  madogo  ambayo  hofu  hujaribu kuingia  na kuniletea  shida.  Alinionyesha kuwa katika  kila hali, haijalishi ukubwa au udogo wake, suluhisho la hali hiyo lilikuwa ni maombi.

Usiogope, kwa  maana ni pamoja nawe; usiangalie  huku  kule kwa hofu na kutahayarika,  kwa maana mimi ni Mungu wako.  Nitakupa nguvu wakati wa magumu,  nitakusaidia. Nitakuinua kwa mkono wangu wa kuume… Isaya 41:10,13 Katika maandiko  haya, Bwana anawaambia watu wake wasiangalie huku na huko wakiwa na hofu au wasiwasi, kwa maana yeye ni Mungu wao. Wakati  mwingine sisi huogopa tunapoangalia  hali ambayo tumo ndani  yake. Haya ni makosa.  Jinsi  tunavyoendelea kukaza macho yetu na midomo  yetu kwenye shida,  ndivyo  tunavyoendelea kushikwa na hofu. Badala yake, tunafaa kuweka macho yetu na midomo yetu juu yake Mwenyezi Mungu.

Yeye anaweza kutatua lolote ambalo litatujia katika maisha haya. Mungu ameahidi kutupatia  nguvu, na kutuimarisha katika magumu, kutuinua na mkono wake wa kuume. Anatuamrisha pia tusiwe na hofu.

Lakini kumbuka, yeye hatuamrishi tusihisi hofu au woga, bali tusikubali hofu au woga ututawale. Mungu anatuambia mimi  na wewe, “Usiogope,  nitakusaidia.” Lakini hatuwezi kuupokea msaada  wa Mungu  mpaka tutakapojiachilia na tuwe watiifu na kutenda atuambialo kwa imani. Je, unajua ni wakati gani ninahisi upako wa kuhubiri? Ni wakati ninapopanda jukwaani nianze kuhubiri—si kabla ya kuanza. Mungu anatuambia  leo, “Acha kukubalia  hofu itawale  maisha yako.”  Anza kufanya yale ninayokuambia ufanye, kwa maana ninayokuambia ni kwa faida yako mwenyewe.

Ninajua baraka zilizo  ng’ambo  ya pili, lakini ibilisi pia anazijua.  Hii ndio  sababu anakupinga kwa kutumia hofu  na  ndio  sababu mimi  ninakuambia usiogope.
” Usiogope, Wewe Ni Wangu! …

Hivyo asema Bwana, aliyekuumba,  Ee Israeli, aliyekutengeneza Ee  Yakobo; usiogope kwa maana nimekukomboa; nimekuita kwa jina lako, wewe ni wangu. Utakapopita kwenye maji,  nitakuwa nawe; utakapopitia mito, haitakugharikisha. Utakapopita kwenye moto, hutachomeka, na miali ya moto haitakuunguza. Isaya 43:1-2. 

Bwana  anatuambia hapa tusiogope wakati tunapopitia majaribu ya kila aina. Hii inamaanisha  kwamba tutapata ushindi  katika maisha yetu,  lakini itakuwa ni wakati tunapopitia  mambo hayo. Kuweza kupitia mambo hayo, ni lazima tuamue kwamba hatutakimbia mbele ya majaribu tena. Bwana ameahidi  kuwa nasi na kutuweka salama  wakati tunapopitia maji mengi ambayo hayatatugharikisha na tunapopitia moto ambao hutatuunguza au kutuchoma.

Je, unaikumbuka hadithi ya wale vijana  watatu wa Kiebrania walioitwa Shadraka, Meshaki na  Abednego? Walitupwa katika tanuru ya moto mkali lakini hawakuumia kabisa. Hawakuwa hata na harufu ya moto. (Danieli 3:1-30). 

Kuna hofu za kutisha, kama ya kutupwa katika tanuru la moto— na kuna hofu ndogo ndogo, kama kuogopa kwamba nywele zako hazitatengezwa vizuri! Unaweza kuwa unaogopa kitu kikubwa kama vile kansa au mshtuko  wa  moyo au kifo cha  mpendwa  katika jamii. Au  unaweza kuwa unaogopa kitu  kidogo kama mvua wakati  wa matembezi au kukosa mahali pa kuegesha gari lako.

Haijalishi chanzo au ukubwa wa hofu yako, ni lazima hofu hiyo itatuliwe  kwa njia ile ile. Kama tulivyoona,  ni lazima ikabiliwe kwa maombi na neno la Mungu. Na wakati tunapoomba, ni lazima tuamini. Hofu ni adui yetu na tunatakuwa kuichukulia kuwa adui.


No comments:

Post a Comment