Sunday, 27 May 2018

KAMA NINGEJUA


Mtume Paulo katika kitabu cha  Wafilipi 3:13 anasema tuyasahau yaliyo nyuma na tuyachuchumilie yaliyo mbele.  



Tunashikilia yaliyopita kwa njia gani ila katika mawazo yetu?  Ninaamini kuwa tunaweza kubingirisha maisha yetu ndani ya mambo ya kale mawazoni badala ya kutumia nguvu hizo kuishi maisha leo. Je, wewe hujikumbusha makosa yako ya kale tena na tena? 
Wewe husema mawazoni mwako, “Kwa nini nilifanya hivi na vile? Ole wangu,  kama singalisema  hivi au  kama singalitenda vile.”  Au, “kama ningalifanya hivi na vile.”  Jihadhari sana na  “kama ingalikuwa.” Labda ulidhani ulikuwa ukifanya kila kitu vyema ilivyotakikana, lakini baadaye matokeo yake yakawa machungu. 

Unaweza kushangaa “kwa nini mambo yalitokea jinsi hii? Kwa nini Mungu? Kwa Nini?  Sielewi.  Lazima nitatue mambo haya.  Siwezi kuvumilia kutojua!  Lo!  Nimechanganyikiwa ajabu!” Je, mawazo yako huwa kama haya?  Nitakuwa wazi nawe.  

“Unajitesa!” Nilijitesa hivi miaka mingi.  Fikra kama hizi  hazisaidii  lolote!    Nilikuwa na mambo zamani, na hata sasa yapo, ambayo sikuelewa wala sijayaelewa hadi sasa. Lakini ninamshukuru Mungu kwa kuufi kisha ujumbe wake kwangu kwamba niache yaliyopita na kuyachuchumilia yaliyo mbele.  Sasa hivi ninaburudika katika amani ya Mungu.

Neno katika Isaya 26:3 linasema, Mungu “atamlinda yeye ambaye moyo wake umemtegemea katika amani kamilifu.” Halisemi kuwa Mungu atamlinda na kumpa amani yule ambaye anashughulisha mawazo yake kuwaza na kuwazua, na kujaribu kutatua kila kitu. 

Mara nyingi, mambo mabaya yasiyo ya haki huwatendekea watu wema. Katika maisha yangu na pengine katika maisha yako ya kale pia, kulikuwa na mambo mengi niliyotendewa ambayo hayakustahili– mambo yaliyoniletea shida nyingi, vidonda na maumivu moyoni mwangu, na imenichukua  miaka mingi kupona.  Nilitumia miaka mingi nikibeba kujihurumia mabegani - nikiwa na uchungu na chuki moyoni.  Nilikuwa nikijaribu kuwazua sababu za mambo yaliyonitendekea. Mbona Mungu hakunisaidia?  Mbona hakuna mtu yeyote aliyenisaidia?” Mwishowe niligundua kwamba nilikuwa nikijihuzunisha bure.  Nilikuwa nikiharibu ‘siku ya leo’  kwa kujaribu kuelewa yaliyopita. Mungu alinena nami siku moja  akisema, “Jimmy, unaweza kuwa mtu wa kujihurumia au mtu hodari.  Unataka yupi?” Wakati mwingine unaweza kuishi katika ushindi wa jana. 

Unaweza kujifunga katika mawazo ya kufikiri jinsi ulivyoshinda jana, na kujaribu kurudia ulichofanya ili upate ushindi tena.  Zamani nilipenda kushikilia ushindi wangu wa kale.  Hata hii inaweza kukuzuia kuenda mbele.   Ya kale ni ya kale.  Hata kama ya kale yalikuwa ya ushindi au kushindwa, ni ya kale.   Yamekwisha.   Ishi siku ya leo! Hakuna kosa katika kuwaza mazuri yaliyopita, lakini ni kosa, tena kosa kubwa kukaa pale.  Baada ya kila kitendo maishani mwako, acha pazia ianguke nyuma yako na uendelee katika yale Mungu amekukusudia.  Wafilipi  3:13  (AMP)  inasema, “… tukisahau yaliyopita na kujisukuma mbele kwa yale yaliyo usoni.”

Ninataka tena kukuonya, jihadhari na kusema  “kama ningejua.”   Ikiwa kitu kibaya kilitendeka, basi tunaanza kufikiri,  “kama singalifanya vile.”  Na ikiwa kitu kizuri kilitendeka, tunajikuta tukifikiri  “kama nilingalifanya vile tena.” Sahau yaliyopita!   Usijaribu kuwaza na kuwazua tena.   Amua sasa kwenda mbele.

No comments:

Post a Comment