Friday, 20 July 2018

Tazama Baraka zako Badala ya Matatizo yako

Siku moja nilisikia  hadithi ya mwanamume mmoja aliyepoteza funguo jioni moja. Basi akawa anazitafuta  sana, alizitafuta  kwa hasira nje  pembezoni mwa moja ya  barabara,  chini ya  mlingoti wa taa  za barabarani.  Mpita njia mmoja  aliona jinsi  alivyokuwa akizitafuta  kwa bidii na akasimama  kumsaidia  kutafuta  funguo hizo.

Baada  ya  dakika chache  za kutafuta  kwa bidii, yule  mgeni aliyekuwa anamsaidia alimwuliza akasema, “Sasa, hizo funguo umeziangusha wapi haswa? Kama tukijua ni wapi haswa,  huenda tukawa na bahati  tukaziona.” Bila  kusita, yule mwenye  funguo zilizopotea  alijibu,  “Niliziangusha  wakati  nilipokuwa  nyumbani kwangu.” Yule mgeni aliyekuwa anamsaidia akapigwa na bumbuazi kusikia  jibu hilo, akasema kwa  mshangao, “Ikiwa umeziangusha nyumbani  kwako, mbona unazitafuta  hapa chini ya mlingoti  wa taa?”  Yule  aliyepoteza  funguo  akajibu,  “Kwa  sababu  hapa  kuna mwangaza zaidi.”
Yamkini  unasema  Huu  ni upuuzi. Kila mtu  anajua kwamba  si jambo la  busara  kufanya  hivyo.  Linaweza  kuonekana  jambo  la  kipumbavu kutafuta  funguo zilizopotea  nyumbani  kwako  chini ya mlingoti wa taa  za barabarani,  lakini ninayo sababu ya kuwasimulia hadithi hiyo.

Mara nyingi  katika maisha,  tunatafuta  kitu tunachohitaji, lakini tunakitafuta  mahali  pasipo sahihi. Kuna wimbo mmoja wa zamani unaosema “looking for love  in all  the  wrong places-Kutafuta mapenzi  mahali  pasipofaa.”  Nadhani  wimbo  huo  unasema  ukweli. Lakini  pia  ninadhani  kuwa  mara  kwa  mara  huwa  tunatafuta matumaini mahali pasipofaa.

Ikiwa kweli  tunataka  kufurahia maisha, itabidi  tufanye mabadiliko ya kimsingi  ya pale  tunapotafuta  matumaini. Sharti Yesu  awe  chanzo  cha  matumaini  yetu  wakati  wote.  Haijalishi  hali zetu  ni za aina  gani. Hali  zetu  hazipaswi kuwa ndivyo vitu vinavyochangia kiwango chetu  cha furaha.  Hata  ikiwa tunaishi katika  siku  mbaya sana, tunaweza  kuwa na mtazamo uliojaa  kujiamini, furaha,  na matumaini ikiwa  tutajifunza kuangalia kile tulichosalia nacho, si kile tulichopoteza. Wakati  wote  angalia  kile  anachofanya Mungu, si kile unachofikira hafanyi. Natamani  mtu  angeliniambia  ukweli  huu  mapema  maishani mwangu. 

Kwa miaka  mingi  nilikuwa  Mkristo wa kuteseka, anayesumbuka,  na moja ya sababu hizo ni  kwamba nilikuwa  wakati wote  nafikiria  juu  ya  kile  nilichokuwa  sina.  Nami  sikufikiria  tu,  bali nililalamika  juu  yake.  Ningetumia  muda  wangu  wa  kuomba  na kumwambia Bwana  mambo yote  niliyokuwa sina.  Mungu, sina  pesa za kutosha.  Sina talanta  ile waliyo nayo wengine.Orodha  ya  mambo  haya  ni  ndefu.  Nilitazama  hapa  na  pale na kufanya hesabu ya kila kitu nisichokuwa nacho. Lakini  Bwana  alianza  kunionyesha  kuwa  nilikuwa  na  vingi tu,  nilikuwa natazama  mahali  pasipofaa.  Hakuna ushindi  katika kuangazia vitu ulivyopoteza au usivyokuwa navyo.

Badala ya kuweka nguvu na juhudi zangu katika  kulalamika juu ya  vile  nilivyopoteza, Bwana alianza kunifundisha  kuangazia vile nilivyosalia navyo. Huenda  sikuwa  na  pesa  nyingi kiasi cha  kuweza  kuwenda  likizo  ya kupendeza  sana, lakini angalau  nilikuwa na pesa za kulipia madeni yangu  ya  mwezi  huo.  Huenda  sikuwa na uwezo  ule  waliokuwa nao watu wengine, lakini nilikuwa mnenaji mzuri, na hatimaye Mungu akaanza  kutumia  kipawa  hicho  kuwasaidia  watu.
Mambo haya  haya  yanaweza  kuwa yametokea  kwako.  Haijalishi unapitia  mambo  gani  leo,  unaweza  kugundua furaha  mpya  katika maisha.  Huenda  umepoteza  mambo  fulani;  huenda  kuna  faida fulani  ambazo  huna.  Lakini  badala  ya  kuangazia  kile  ulichopoteza, kwa nini usitafute  miongoni mwa kile  ulichosalia nacho? Unaweza ukashangaa kwa kile utakachokiona.

No comments:

Post a Comment