Tuesday, 3 July 2018

Mwelekeo wa Hofu.

Kukumbana na mabadiliko makuu maishani  ni moja  ya mambo magumu zaidi ambayo tumeitwa kuvumilia. Hata kama ni sisi wenyewe tuliochagua  kuwa na mabadiliko hayo, haimaanishi ya kuwa mambo hayo yatakuwa rahisi kwetu. Ikiwa mabadiliko haya yanatokana na msiba, kifo au pigo fulani, basi kuhisi kuchanganyikiwa, kupoteza mwelekeo,  na hofu ni kawaida.  Kwa  sababu  ghafla  mipango  yetu  ya  usoni  inaangamia.Safari ya mapumziko, mpango wa kununua nyumba, pesa za malipo ya uzeeni au mipango mingine ya maana sana kwetu ghafla inaangamia. Inachukua muda mrefu kwetu kupata mwelekeo mpya. Katika nyakati  kama hizi, maswali mengi huja katika  mawazo yetu, mengi yao yanayohitaji majibu papo hapo. Hata  jamaa  na  marafiki  wanaweza  kuwa  wanauliza  tena  na  tena, “Utafanyaje sasa?  Utaishi  wapi sasa?  Utarejea  kazini mara  moja  au utachukua muda kupumzika?” Yote haya ni maswali mema ambayo mwishowe lazima yajibiwe. Iwapo umepatwa na msiba au pigo ambalo limebadilisha maisha yako,  unajua unahitaji  kufanya  uamuzi katika  sehemu kadhaa za maisha yako kuhusu siku za usoni.

Lakini unaweza kuwa unajihisi kwamba huko tayari kufanya hivyo! Nyakati  kama hizi, huwa umejawa na mawazo mengi ya kutatanisha.  Unaweza kufanya  uamuzi fulani, kisha ghafula ukabadili nia kuhusu uamuzi huo. Hisia zako zinaanza kukufanyia mzaha; mara unataka hili mara unataka lile. Inakuwa ni vigumu kufanya uamuzi ukiwa katika hali hii kuliko nyakati za kawaida. Mara nyingi wakati umechanganyikiwa na kukosa mwelekeo hivi, hofu hukuvamia pia. Unaweza kuanza kujiuliza maswali  kama haya, “Nitafanyaje kuhusu fedha zangu? Ni nani atakayeanza kushughulikia mambo haya ambayo sijazoea kuyashughulikia?” Unapokuwa umebanwa na mambo kama haya, ninakuhimiza uyatafakari maneno haya kutoka kitabu  cha Waebrania.


Maneno haya hunipatia  faraja na tumaini, nami naamini yatakutia  moyo pia: Mungu mwenyewe  amesema:  “Sitakuacha kamwe,  wala sitakutupa.” Waebrania 13:5 Tunapokuwa hatujui cha kufanya au yale ambayo yanatungojea baadaye, ni jambo la kufariji kumjua yule ayajuaye mambo  hayo. Katika Zaburi 139:15-17, mtenzi anatuhimiza kuwa Baba yetu wa mbinguni anajua maisha yetu ya kale, ya sasa, na ya baadaye: Umbo  langu  halikufichika  kwako  nilipokuwa  ninatungwa  ndani ya tumbo la mamangu. Wewe uliniona hata kabla  sijazaliwa, uliandika kila kitu  kitabuni mwako; siku zangu zote ulizipanga, hata kabla ya kuweko ile ya kwanza. Ee  Mungu, mawazo  yako ni makuu mno;  hayawezi kabisa kuhesabika! Mungu ndiye Alfa na Omega, mwanzo na mwisho. Na kwa sababu hii ni kweli, yeye pia ndiye kila kitu kilicho katikati  ya  Alfa na Omega. 

Anajua  hali zetu naye atatuongoza na kutuelekeza iwapo tutamtegemea afanye hivyo. Baba yetu  wa mbinguni  kwa kawaida hutupatia  kile tunachohitaji kuweza kuishi siku kwa siku. Neema  ya kuishi katika siku moja hutujia siku hiyo inapoanza. Kwa sababu hii, ni vigumu kuyawazia maisha ya baadaye kwa muda mrefu, bila kuhisi woga. Tunapowazia maisha ya baadaye, sisi huhisi ya kwamba hatuwezi kukumbana na  shida  ambazo  zinaambatana na siku  hizo. 

Lakini hii ni kwa sababu sisi  huwa tunazitazama siku hizo bila neema ya Bwana juu yetu. Tunapofikia  mahali  au  siku  fulani,  tutaikuta  neema  ya  wakati  ule mahali pale. Kwa maelfu  ya miaka,  Zaburi 23  imewahudumia  na  kuwafariji mamilioni  ya watu ambao wamekuwa wapweke na wenye kuomboleza. Wakati  wa kuchanganyikiwa,  kupoteza  mwelekeo na kuwa na hofu nyingi, wewe tumia maandiko haya kama nanga ya nafsi yako: Bwana ndiye Mchungaji wangu, sitapungukiwa kitu, yeye hunilaza katika majani mabichi, huiongoza kwenye maji  matulivu.  Huirejeza na kuipumzisha nafsi yangu, huniongoza kwenye  njia za haki - kwa ajili ya jina lake.  Nijapopita katika bonde la uvuli wa mauti, sitaogopa, kwa maana u pamoja nami. Fimbo yako na gongo lako huniongoza.  Umeniandalia karama machoni pa watesi wangu, umenipaka mafuta kichwani mwangu. Kikombe changu umekijaza mpaka kufurika.   Hakika  wema na fadhili zitanifuata mimi,  siku zote za maisha  yangu nami nitakaa nyumbani  mwa Mwenyezi - Mungu milele.

No comments:

Post a Comment